MDAU POPOTE ULIPO TUMA PICHA NA HABARI KWA E-mail:  antonysiame74@yahoo.com

Tuesday, September 12, 2017

TUME YA HAKI ZA BINADAMU YAMPONGEZA JPM




Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu,  Bahame Tom Nyanduga,
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imepokea tamko la  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alilolitoa Septemba 11, 2017 kuhusu kutotekeleza adhabu ya kifo wakati wa uongozi wake, kuwa ni tamko lenye kuzingatia haki ya msingi ya kuishi.
 Tume inapenda kuungana na wadau wengine kumpongeza  Rais kwa tamko hilo ambalo limekuja muda mfupi kabla ya Siku ya Kimataifa ya kuhamasisha nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kufuta adhabu ya kifo, ambayo huadhimishwa Oktoba 3 ya kila mwaka. 
 Uamuzi wa  Rais unaendana na Mkataba wa Kimataifa na maazimio ya Umoja wa Mataifa yanayozitaka nchi wanachama kufuta au kusimamisha utekelezaji wa adhabu ya kifo (abolition/moratorium on the death penalty).
 Tume inatambua kwamba adhabu ya kifo haijatekelezwa hapa nchini katika kipindi cha takriban miaka 20 iliyopita na hivyo kudhihirisha kwamba Tanzania ni nchi isiyotekeleza adhabu ya kifo kwa hiari yake yenyewe pamoja na uwepo wa adhabu hiyo katika sheria za nchi.


Kwa kuzingatia kauli ya Rais pamoja na mahitaji ya sheria za kimataifa za haki za binadamu, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inapenda kuchukua nafasi hii, kuishauri Serikali iridhie Itifaki ya pili ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa; Itifaki ambayo inazitaka nchi wanachama kufuta adhabu ya kifo.






No comments:

Post a Comment