MDAU POPOTE ULIPO TUMA PICHA NA HABARI KWA E-mail:  antonysiame74@yahoo.com

Monday, January 16, 2012





 
HOTUBA YA KAIMU MWENYEKITI WA UMOJA WA VIJANA WA CHAMA CHA MAPINDUZI (UVCCM), NDUGU BENNO MALISA KWA MAKATIBU WA VIJANA WA WILAYA ZOTE NCHINI, DODOMA, 15 JANUARI 2012

Mh Katibu Mkuu wa CCM

Mh Katibu mkuu wa Uvccm

Mh Naibu katibu mkuu Uvccm Znz

Mh wakuu wa Idara makao makuu Uvccm

Mh Mwenyekiti Mwenyeji

Waheshimiwa Makatibu wa Uvccm Mikoa na wilaya

Waheshimiwa Watendaji wa Chama wa Mkoani Dodoma

 Waheshimiwa watoa mada,Wageni waalikwa Mabibi na Mabwana


Kwanza niwashukuru kwa kuitikia wito wetu ikiwa ni utekelezaji wa maazimio ya Vikao vyetu pamoja na Vya Chama ikitutaka tuwe na semina ya namna hii kabla ya uchaguzi mkuu wa Jumuiya na Chama.

Tumekua jumuiya ya kwanza kutekeleza agizo la chama kwahiyo hatuna Budi kujipongeza.

Pili tumshukuru mwenyezi mungu kwa kuweza kuoona mwaka mpya na kutufikisha sote salama hapa Dodoma pamoja niwatakie heri ya mwaka mpya .
 Napenda kuwakaribisha vijana wenzangu na viongozi wote wa Wakati nikitoa shukrani zangu hizo, napenda kutumia fursa hii kuwapa pole nyingi sana vijana wenzetu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kutokana na kifo cha ghafla kilichotokana na ajali ya gari kilichomkuta kijana mwenzetu, Mbunge wa Viti Maalum, Regia Mtema. Tunaomba Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu pema peponi.

Malengo ya semina hii  ni kama alivoeleza katibu mkuu hapo awali kuwa ni kukutana na watendaji ,kuweka mkakati wa pamoja wa uchaguzi wa jumuiya na chama kujadili ratiba,kanuni na utaratibu mzima wa uchaguzi mwaka huu.

Wakati huo huo tutajadili uchumi jumuiya,changamoto zinazotukabili vijana,hali ya watendaji wetu na maslahi yao kwa ujumla,Vile vile kupitia kikao hiki tutatoka na maazimio ambayo tutawekeana muda maalum juu ya utekelezaji wake.


Ndugu zangu, tunakutana leo hapa Dodoma wakati taifa na jumuiya yetu ya vijana vikipita katika kipindi ambacho vikikabiliwa na changamoto nyingi pengine kuliko ilivyopata kuwa wakati mwingine wowote.

Katika ngazi ya kitaifa changamoto hizo zimesababisha kuibuka kwa kila aina ya majina yanayojaribu kueleza au kufafanua mahali ambako kama taifa tumefikia kuwapo sasa.

Wako ambao wanasema taifa liko njia panda huku wengine kwa sababu tu ya kujawa na hofu wamefikia hatua ya kuielezea hali tuliyomo leo kama kipimo cha kutoweka kwa matumaini ya kitaifa au hata kukatisha tamaa.

Ndani ya jumuiya yetu, mitazamo imekuwa ni hiyo hiyo ya baadhi yetu na hata wale walio nje kufikia hatua ya kutuona kuwa watu tuliopoteza mwelekeo, tuliosambaratika, tuliopoteza matumaini na/au watu ambao tumepoteza dira ya kuendelea kuwapo kwetu kama moja ya jumuiya za chama iliyo na nguvu na ushawishi mkubwa.

Tutakuwa ni watu wa hovyo na viongozi wa ajabu iwapo sisi wenyewe tutajifanya eti kuzipuuza hofu za namna hii zinazoelekezwa kwa taifa letu na hata kwetu sisi tuliopewa dhamana ya kuiongoza jumuiya yetu wakati huu.

Tunayo sababu kubwa moja ya kutozipuuza hata kidogo changamoto mbalimbali zinazowajengea Watanzania wenzetu hofu za namna hii, nayo si nyingine zaidi ya ukweli kwamba, sisi ndiyo vijana tunaotokana na chama kilichokabidhiwa na wananchi dhamana ya kuliongoza taifa hili.

Tukiwa kundi kubwa zaidi la kijamii ndani ya chama na hata katika taifa kwa ujumla, sambamba na kutambua kwetu kwamba katika rika letu sisi ndiyo nguvu kazi kubwa zaidi kuliko ilivyo kwa kundi jingine lolote, tunapaswa kujiona na kutambua kwamba, tunayo dhamana kubwa kwa chama chetu, serikali na kwa taifa kubwa. 

Dhamana ninayozungumzia hapa si nyingine, bali ni ile inayotupasa kuwa na majibu, tena majibu sahihi na makini yatakayotoa mwelekeo na kumaliza kila aina ya hofu wanazokabiliana nazo wana CCM na Watanzania kwa ujumla.

Dhamana tuliyonayo ni ile ya kuhakikisha tunakuwa mstari wa mbele kulinda, kusimamia na kuendeleza mafanikio ya kihistoria, kimaadili na kimaendeleo ya taifa letu ambayo tumeyapata katika kipindi chote cha miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara na 48 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Si hayo tu, dhamana nyingine tuliyonayo tukiwa vijana ni kuhakikisha sisi wenyewe tunakuwa chachu ya kuhakikisha viongozi wa kisiasa na kiserikali wanaotokana na chama chetu wanazingatia na kuheshimu maadili ya msingi ya kiuongozi ya CCM wakati wote wanapotimiza wajibu wao.

Ni wazi kwamba ili tuweze kutimiza ipasavyo wajibu huo, sisi wenyewe vijana tunapaswa kuthibitisha pasi na shaka kwamba malezi na makuzi ya kisiasa, kiuongozi na kimaadili ndiyo yanayotupa jeuri mamlaka ya kusema au kufanya kile tunachokifanya kwa bidii na kwa kujiamini.

Tutakuwa tukijidanganya wenyewe iwapo tutakuwa na fikra kwamba tutaweza kutimiza wajibu wetu ipasavyo iwapo tutajiingiza katika vitendo vya rushwa, matumizi ya madawa ya kulevya au katika matendo mengine yoyote yanayoweza kutupotezea uhalali wa kiuongozi.

Ndugu zangu wakati tunapokutana leo, sisi viongozi wa vijana, wale wa chama chetu na serikali kwa ujumla tunakabiliwa na shinikizo kubwa la lawama kutoka kwa mahasimu wetu wa kisiasa, wanaharakati na kutoka katika vyombo vya habari.

Lakini katika mazingira ambayo yumkini yanadhoofisha mshikamano na misingi ya uwajibikaji wa pamoja katika jumuiya, ndani ya chama na hata serikalini umeibuka utamaduni mpya na wa hovyo kabisa wa viongozi kupakana matope, kuzushiana na kurushiana lawama hadharani na katika namna inayoibua hali ambayo sisi kama vijana hatuna sababu ya kuogopa kuizungumzia.

Utamaduni huu ambao umetoa fursa hata kwa wapinzani wetu kutushambulia umechukua picha ya wana CCM wenyewe kwa wenyewe na wakati mwingine mawaziri kusutana kupitia katika vyombo vya habari na kwenye mikutano ya hadhara kwa namna inayokiumiza zaidi chama kuliko kukijenga.

Watu wanaofanya hivyo wanapoulizwa kulikoni wamekuwa wepesi wa kujificha nyuma ya vivuli mbalimbali vikiwamo vile vya eti kutumia uhuru wao wa kidemokrasia wa kutoa maoni au wa kuuonyesha umma kwamba wanafanya hivyo kwa nia safi ya kukabiliana na vitendo vya rushwa na ufisadi vilivyokithiri miongoni mwa jamii kivulu kikubwa wanachojivalisha ni UZALENDO.

Ingawa hili halijawekwa wazi na kuchunguzwa kwa kina, utamaduni huu wa viongozi kutumia vibaya uhuru wa kidemokrasia katika kukwepa vikao halali katika kufikisha hoja zao umekuwa unaotuumiza zaidi kuliko unavyotusaidia kama jumuiya na kama chama.

Hulka za namna hii ndizo ambazo leo hii zimesababisha nyufa zilizo dhahiri ndani ya jumuiya yetu, miongoni mwa makada na viongozi wa chama chetu na hata kati ya viongozi wa serikali kwa ujumla.

Ni jambo la bahati mbaya kwamba, hata baada ya chama kutoa agizo lililokuwa likiwakumbusha viongozi na makada kutumia vikao kufikisha hoja zao badala ya majukwaa mengine ya hadharani, bado utamaduni huu umeendelea pasipo kukemewa.

Wala hatuhitaji wanazuoni kutoka nje ya chama chetu kuja hapa leo na kutueleza madhara ambayo kama jumuiya na kama chama cha siasa tumeyapata kutokana na makosa na udhaifu wetu wa kuendelea kuulea utamaduni huu ambao hatuna budi kuchukua hatua za makusudi kuukemea na kuulaani kwa nguvu zetu zote.

Uongozi ni kuonyesha njia. Kwa sababu ya kutambua athari zinazotokana na kuendekeza kwetu utamaduni huo, mimi naona niwe kiongozi wa kwanza kuwaasa viongozi wenzangu wa jumuiya hii yenye nguvu ya chama kuanza kuchukua hatua za kuwakemea kwa uwazi viongozi wote ambao wataendeleza utamaduni huo.

Wito wangu kwa viongozi wenzangu ni kulijadili hili kwanza katika mkutano wetu huu kabla ya kutafuta namna bora ya kuja na azimio ambalo litatuongoza katika kukemea na kulaani vitendo vya namna hii wakati tutakapokuwa tumerejea katika maeneo yetu ya kazi.

Waswahili wanao msemo usemao; ‘wakati ukuta’ ambao una maana kubwa moja kwamba katika lolote unalofanya unapaswa kuhakikisha unalifanya katika majira na wakati unaopaswa.

Bado tunao muda wa kutosha wa kujipanga upya kwa nia ya kusahihisha makosa makubwa ambayo tumeyafanya kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa ndani ya chama baadaye mwaka huu na uchaguzi mkuu mwaka 2015.

Tutaweza kufanya hivyo iwapo tutaukumbuka ushauri aliopata kuutoa mwenyekiti wetu mstaafu wa CCM, mzee wetu, Benjamin Mkapa wakati alipohutubia mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Agosti mwaka 2004.

Katika hotuba yake hiyo iliyokuwa na kichwa kisemacho ‘Ushupavu wa Uongozi’, Mzee Mkapa aliwaasa wana CCM kuwa makina na kukinusuru chama chao kujiingiza katika hatari ya ajenda zake kuandaliwa na vyama vya upinzani na vyombo vya habari wakati kikijiandaa kuingia katika uchaguzi.

Msema kweli ni mpenzi wa Mungu, maneno hayo ya Mzee Mkapa yana maana sana leo kuliko ilivyokuwa miaka takriban saba iliyopita wakati alipoyatoa.

Hakuna asiyejua kwamba, leo hii viongozi wa kisiasa na kiserikali wanaotokana na CCM ndiyo ambao tumekuwa mstari wa mbele katika kuzibeba juu juu hoja za magazetini na zile za wapinzani wetu na kuzitumia kama ajenda za kujijenga kwetu kisiasa.

Mwenye macho haambiwi tazama. Sina sababu ya kuzitaja hapa hoja za wapinzani ambazo tumezishabikia na kuzikumbatia kwa gharama za ustawi na heshima ya chama chetu katika jamii.

Hivi ni nani hajui kwamba, utamaduni huu wa kuiga na kuyadaka pasipo kuyachuja na kupima kwa kina masuala yanayoandikwa magazetini au yale yanayosemwa katika majukwaa na viongozi wa vyama vya upinzani ndiyo ambayo yamekigharimu chama chetu kabla na hata wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka juzi?

Je, tutakuwa tukijitendea haki sisi wenyewe, chama chetu na serikali yetu iwapo tutaendelea kuwa watazamaji na kukubali kuzama kwa sababu ya kuwaacha wanaoutoboa mtumbwi tulioupanda? Jibu ni hapana. Tunapaswa kuchukua hatua za kujisahihisha sasa

Ndg zangu zipo changamoto kubwa zinazotukabili ambazo nilazima nizisemee hapa leo.




Ajira kwa vijana
Tatizo la ajira linaikumba dunia na Tanzania pia. Vijana wengi wako mtaani si kwa kupenda, lakini hawana ajira. Ni vizuri sasa watendaji wa UVCCM na chama tukaanza kuweka mkakati endelevu kubuni mbinu za kuzalisha ajira kwa vijana wetu ambao ni zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wote.
Vijana hawa wasipopatiwa ajira kwa kubuniwa mpango wa kuanzishwa kwa viwanda hawatatuelewa kamwe katika Uchaguzi Mkuu ujao. Lazima ndugu zangu tatambue ukweli kwamba katika Uchaguzi Mkuu ujao watakaoamua nani au chama gani kichukue dola ni vijana maana watakuwa zaidi ya asilimia 50 ya wapigakura wote.

Ndio maana nawaasa viongozi wa chama,  tuache malumbano ambayo haina manufaa kwa vijana na tuanze mkakati maalum wa kumsaidia kijana wa Kitanzania. Lazima tufike mahali tutambue kwamba hata kijana wa UVCCM kama hana ajira hawezi kuwa mfuasi wako kwenye uchaguzi ujao na wala hawazi kuwa RAIA katika Taifa lake, Serekali ya CCM imewapa ELIMU kuanzaia shule za msingi,sekondari na elimu ya JUU ingawa kuna changamoto kubwa ambazo lazima zipate majibu na ufumbuzi wa kisera na kimkati katika ELIMU ya Juu hasa swala mikopo, Sekondari has aswala la waalimu na ,maabara na Ubora wa Elimu katika shule zetu za sekondari hasa za KATA.

Hili halikwepeki kwakua sisi ji sehemu ya Dunia na Tanzania,matatiuzo haya ni yetu sote Ajira inamuathiri kila Kijana na Kijana wa CCM nae ni muathirika tusidhani sisi si sehemu ya ,matatizo.

Ndg kwa kutambua hili ninaagiza mikoa ya RUKWA,MBEYA,RUVUMA,IRINGA,MOROGORO,DODOMA,SINGIDA,TABORA,KIGOMA,KAGERA,MWANZA,MARA,LINDI,MTWARA,MANYARA,KASKAZINI PEMBA,KASKAZINI UNGUJA kila wilaya kufikia mwezi wa pili mwaka huu Tarehe 15  kamati za utekelezaji zikutane na waaalike wakuu wa wilaya,na wenyeviti wa halmashauri katika maeneo ambayo hatuna wenyeviti wa halamshauri waalikwe wakurugenzi wa halamshauri na kujadili uanzishwaji wa mashamba ya Uvccm na kila wilaya ipate eneo walau HEKAARI 300. Na kwa upande wa Zanzibar walau HEKARI 50,
Jumuiya makao makuu tutakua na jukumu la baada ya upatikanaji wa ardhi tutafanya utaratibu wa ukopaji wa matrekata kwakutumia hati  za mashamba hayo kufikia mwezi wa tano mwaka huu zoezi hili liwe limekamilika kitaifa.
Kupitia mashamba haya tutahakikisha yanakua ni sehemu ya kuleta ajira kwa Vijana na sisi kuwa sehemu ya kupunguza tatizo  hilo Mfumo wa uendeshaji wa mradi huu utaandaliwa na mimi Binafsi nitaanza ziara katika mikoa niliotaja na kupita kila wilaya kuanzia mwezi wa Pili tarehe 25th.
UCHUMI WA JUMUIYA.
Ndg zangu jumuiya yetu imepita katika kipindi kigumu toka enzi za kina Guninita,Dk Emanuel Nchimbi na SASA lakini tunakila sababu ya kumshukuru Dk Nchimbi,Uongozi wote uliopita Chini ya Baraza la wadhamini linaloongozwa na Waziri mkuu Mstaafu Ndg Edward Ngoyai Lowasa kwa kutusaidia kuanzishwa kwa Mradi wa Majengo PACHA ya UBIA ambayo yataifanya Jumuiya hii kuwa ya kwanza kujitegemea kiuchumi,tulitukanwa sana na kudhalilishwa kwa MRADI HUU na baadhi ya Viongozi wenzetu wa chama lakini leo niwaambie ushirikiano na umoja mlionyesha kama watendaji kuanzia mwezi wa Tano mwaka huu KUOMBA KUMEISHA TUTAKUA JUMUIYA HURU KIUCHUMI.Niwaahidi matunda haya hayatokua ya makao makuu tu bali niyenu nyote na nyinyi mtakua miongozi mwa watu wataokao Faidika,tutaanza kuongeza Kipato chenu mara baada ya mradi huu kuazia kutumika mwezi june.

Niwatakle mikoa na wilaya endeleeni kubuni miradi na kufufua miradi iliyokufa na katika mikoa niliyotaja nitakapoanza ziara yangu kukagua utekelezaji wa mradi huu wa kilimo nintaka kujua miradi hiyo na iliyokufa katika kila wilaya na mkoa.

Katiba Mpya
Mbali na uchaguzi wa jumuiya ndani ya chama, uchaguzi wa chama, kuna suala muhimu sana nalo ni mchakato wa Katiba Mpya ambao Rais wetu mpendwa, Jakaya Kikwete aliuasisi mara baada ya kuchaguliwa kuiongoza nchi kwa mara ya pili.
Hili ni tukio la kihistoria ambao sisi kama viongozi na watendaji wa UVCCM lazima tushikane bega kwa bega na viongozi wetu katika kuhamasisha vijana washiriki kutoa maoni kwa ajili ya kutengenezwa kwa Katiba Mpya. Vijana wa CCM lazima tuonyesha kwamba tuko mstari wa mbele kuhamasisha umma utoe maoni kuhusu Katiba Mpya kwa kuwa ni jambo jema kwa manufaa ya Tanzania ya sasa na ya zaidi ya miaka 50 ijayo.
UCHAGUZI WA CHAMA NA JUMUIYA
Ndugu zangu vijana wenzangu, uchaguzi wa mwaka huu ni muhimu sana katika historia ya chama chetu, ni uchaguzi ambao unaweza kutufanya tukaimarika zaidi mbele ya umma wa Watanzania au kutuboa mbele ya jamii hasa vijana ambao si wanachama wetu, lakini tunawahitaji kwa dhati watuunge mkono katika chaguzi zijazo cha Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Ndugu zangu watendaji,  ni matumaini kwamba uchaguzi huu utaendelea kujenga umoja wetu na kutuweka karibu zaidi na vijana wenzetu kama utafuata taratibu ambazo tumejiwekea na ambazo zinakubalika na Chama chetu Cha Mapinduzi bila kuingiliwa na watu wenye ajenda zao za siri na ambao si wanachama wa jumuiya yetu.
Ndio maana napenda kusisitiza kwamba uchaguzi wa jumuiya ni wanajumuiya kwa maslahi ya chama chetu. Nimeamua kusema haya ili mkioona watu wakipita huko wakiwaambia mchagueni huyu kwasababu ni wa kundi langu, kataeni, waambieni hapa tunachagua viongozi bora wa kuitumikia jumuiya, chama chetu na taifa letu, hatuchagui kundi la mtu hapa kwa ajili ya maslahi yake binafsi.

Ndio maana aliyekuwa Waziri Mkuu wa Uingereza, Tony Blair aliwahi kunukuliwa akisema kwamba  ‘’The art of leadership is saying no, not saying yes. It is very easy to say yes, akiimanisha kwamba kipaji cha uongozi ni uwezo wa kiongozi kusema HAPANA, na siyo kusema NDIO kwa kuwa ni rahisi sana kusema NDIO. Nukuu hii ya Tony Blair ni muhimu sana katika uchaguzi ndani ya jumuiya yetu, tunataka watendaji wetu wafuate amri za kanuni zetu ambazo tumejiwekea na si maagizo ya watu fulani ambao malengo  yao hatuyajui. 

MWISHO
Mwisho ndgzangu katika kipindi change cha uongozi na huu ukiwa ni mwaka wa mwisho mmenipa ushirikiano mkubwa sana ambao umetuwezesha kuvuka mabonde na milima na kwa hilo leo tuko wamoja jumiya yetu haina makundi wapo wachache wanotaka kutuvuruga ndugu zangu mimi nipo Imara tusiwape fursa hiyo tunaelekea katika uchaguzi niwatake vijana wote wenye uwezo na nia njema wajitokeze katika kila nafasi ili tuwe na uwakilishi mkubwa ndani ya chama kujenga JUMUIYA MPYA NA CCM MPYA 2012,Kauli MBIU YETU KAMA JUMUYA NI “ UVCCM MPYA KUELKEA CCM MPYA”
Sntakua kuwa mwema nisimp mshukuru rais jakaya mrisho kikwete na viongozi wa chama wamekua wakitupa ushiorikiano mkubwa katika kufanya shughuli zetu tunampongeza Rais klwa kazi nzuri anayofanya anakumbana na changamoto nyingi niseme kuwa Hayuko peke yake tuko nae na hatuyumbi





No comments:

Post a Comment